Jumanne, 21 Novemba 2017

MAKUNDI MAWILI YA WATU WANAOKUZUNGUKA.

FAHAMU MAKUNDI MAWILI YA WATU KATIKA MAISHA YAKO.
Na Steven Mshiu.
Maisha ya kila mwanadamu yamezungukwa na watu. Watu hawa waweza katika makundi mbalimbali. Waweza kuwa watu wema au wabaya. Hali na vipato vyetu husababisha kutokea mgawanyiko na kutengeneza makundi. Leo nataka nikupe aina mbili za makundi haya.
KUNDI LA KWANZA: KUTOKA NDANI KWENDA NJE:
Hili ni kundi ambalo lipo pamoja na wewe. Nia ya kundi hili sio nzuri hata kidogo. Lipo na wewe pale unapokuwa katika raha tu. Watakula na kunywa vyako. Watatumia kila kilicho chako. Hii ni kwa sababu una kitu. Siku ukiishiwa Kundi hili hutoka upande wako, kwenda nje ya maisha yako.
Halikuthamini tena kwa sababu umefikwa na upungufu. Siku zote hubeba taarifa zako mbaya na kuzipeleka nje. Kama huna akili ya ziada huwezi kulitambua kundi hili hadi pale utakapofikwa na tatizo ndipo utakapofahamu uhalisia wa kundi hili.
KUNDI LA PILI:KUTOKA NJE KUJA NDANI
Hili ni kundi ambalo mara nyingi huwezi kulipa thamani yake. Halipo na wewe pale unapokuwa katika raha au furaha. Pale unapofikwa na matatizo ndipo linapojitokeza. Kundi hili hubeba habari za matumaini. Hubeba habari ya kurejeshwa tena. Hubeba habari za kutia moyo.
Kundi hili hutoka nje na kuja kwako.
Wakati lile kundi la kwanza likitoka kwako kwenda nje na hili la pili linalotoka nje kuja kwako lile kundi la kwanza hujaribu kulivunja moyo lile kundi la pili kwamba mambo yameharibika, Hivyo lisijisumbue kuja kwako. Lakini kwa sababu kundi hili la pili limebeba habari za matumaini huwa halivunjiki moyo.
Luka 8:49-56, Hapa tunaona makundi mawili, moja ni la Yesu lakini la pili ni la waombolezaji. Kundi la Yesu linaletewa habari ya msiba wa binti, Yesu anasema kuwa yule binti hajafa kwani amelala tu, Lakini lile kundi lingine linazipinga habari au taarifa za matumaini zilizotolewa na Yesu za urejesho wa uhai wa binti yule.
Kundi hili lipo pamoja na mfiwa likiomboleza na kulia lakini pale linaposikia habari za binti kurejeshewa uhai linaanza kucheka na kulibeza lile kundi lililotoa habari za matumaini.
Ndivyo ilivyo hata katika maisha yetu, Kuna kundi utaliona lipo pamoja na wewe lakini nia yake ni kukuona tu ukiwa katika hali mbaya. Halipendi kukuona ukiwa umefanikiwa. Halipendi kukuona ukipata kitu. Kupoteza kwako kwao ni furaha. Cha ajabu laweza kuwa ni kundi la wapendwa. Liepuke kundi hili.
Usifikiri kila mtu ni mwema kwako. Kuna ambao wanalia pamoja na wewe lakini mioyoni wao wanacheka. Kuna wanaokutia moyo lakini dhamira zao zinawashughudia kabisa kuwa ni wanafiki. Kuna ambao kwa nje wanaonyesha nyuso za furaha na kufurahi pamoja pale unapokuwa umepata kitu, Lakini mioyoni mwao wana huzuni kuu, kwanini wewe umepata.
Mpendwa rafiki jitahidi ukae upande wa kundi hili la pili. Hili ni kundi lenye habari za mafanikio, Hubeba habari njema. Kundi hili hutokea na kuchukua nafasi inayoachwa na kundi la kwanza.
Mungu akusaidie kuyapambanua makundi ya watu wanaokuzunguka.
Steven Mshiu
0655 882074

Alhamisi, 16 Novemba 2017

Siku sahihi ya kuabudu ni ipi

Swali: "Ni siku gani ya sabato, Jumamosi au Jumapili? Wakristo wastahili kuitunza hii siku?" Jibu: Kila mara husemwa kuwa “Mungu ndiye alianzisha sabato katika shamba la Edeni” kwa sababu ya uhusiano kati ya Sabato na uumbaji katika Kutoka 20:11. ingawa starehe ya Mungu siku ya Sabato (Mwanzo 2:3) iliangazia sheria ya Sabato iliyokua inakuja, hakuna maelezo yoyote ya Bibilia juu ya Sabato kwa watoto wa Israeli kabla watoke Misri. Hakuna maandiko katika Bibilia au dondoo lolote linaloonyesha kuwa Adamu na Musa waliitunza Sabato. Neno la Mungu laiweka wazi kuwa kuitunza Sabato ilikua ishara maalumu kati ya Mungu na Waisraeli: “Kwa ajili ya hayo wana wa Israeli watishika sabato, kuiangalia sana hiyo sabato katika vizazi vyao vyote, ni agano la milele. Ni ishara kati ya mimi na wana wa Israeli milele; kwani kwa siku sita BWANA alifanya mbingu na nchi, akastarehe kwa siku ya saba na kupumzika” (Kutoka 31: 16-16). Katika Kumbukumbu La Torati 5, Musa anazirudia amri kumi kwa kizazi kingine cha Israeli. Hapa baada ya kuamrisha jinsi ya kuitunza sabato katika aya ya 12-14, Musa anatoa sababu ya sabato ambayo sabato ilipewa kwa taifa la Israeli: “Nawe utakumbuka ya kuwa wewe ulikuwa mtumwa katika nchi ya Misri, na akuwa BWANA, Mungu wako, alikutoa huko kwa mkono wenye nguvu, na mkono ulionyoshwa; kwa sababu hiyo BWANA Mungu wako, alikuamuru uishike sabato” (Kumbukumbu La Torati 5:15). Lengo la Mungu kupeana sabato kwa Waisraeli haikuwa kukumbuka uumbaji, bali waukumbuke utumwa wa Wamisri na kule kuokolewa na Bwana. Kumbuka yanayohitajika kwa kuitunza sabato: mtu aliyewekwa chini ya hiyo sheria hangeweza kutoka kwa boma yake (Kutoka 16:29), hangewakisha moto (Kutoka 35:3), angeruhusu mtu yeyote kufanya kazi (Kumbukumbu La Torati 5:14). Mtu mwenye angivunja shreria ya sabato angeuwawa (Kutoka 31:15; Hesabu 15:32-35). Uchunganusi wa ukurasa wa Agano Jipya watuonyesha mambo mane muimu: 1) Popote Kristo alionekena baada ya kufufuka kwake na siku zimetajwa, kila wakati ni siku ya kwanza ya Juma (Mathayo 28:1,9, 10; Mariko 16:9; Luka 24:1,13,15; Yohana 20:19, 26). 2) Wakati pekee sabato imetajwa kutoka kwa kitabu cha Matendo ya Mitume hadi ufunuo ni kwa sababu ya lengo la uinjilisti kwa Wayahudi kwenye Masinagogi (Matendo Ya Mitume 13-18). Paulo aliandika, “Nilikuwa kama Myahudi kwa Wayahudi, ili niwapate Wayahudi” (1 Wakorintho 9:20). Paulo hakuenda kaitka Masinagogi kuwa na ushirika na kuwajenga waumini, bali alienda ili awathibitishie injili na kuwaokoa walikuwa wamepotea. 3) Mara moja Paulo anasema, “tangu sasa nitakwenda kwa watu wa Mataifa” (Matendo Ya Mitume 18:6), sabato tena haitajwi kamwe. Na 4) Badala ya kupendekeza kuwa waitunze siku ya sabato, sehemu nyingine ya Agano Jipya iliyobaki yasema kinyume ( ikijumulisha sehemu ya tatu ilioachwa nche hapo juu, inapatika katika Wakolosai 2:16). Kwa kuingalia hoja ya nne kwa makini, tutafumbua kwamba, hakuna jukumu lolote la kuitunza sabato kwa waumini wa Agano Jipya. Pia tutaonyesha kuwa dhana ya Jumapili “Sabato ya Wakristo” si ya kibibilia. Vile imejadiliwa hapo juu, hakuna wakati sabato imetajwa baada ya Paulo kuanza kuangazia Mataifa, “Basi mtu asiwahukumu ninyi katika vyakula au vinywaji, au kwa sababu ya sikukuu au mwandamo wa mwezi, au sabato; mambo hayo ni kivuli cha mambo yajayo; bali mwili ni wa Kristo” (Wakolosai 2:16-17). Sabato ya Kiyahudi ilifutiliwa msalabani hamali ambapo Kristo “Akiisha kuifuta ile hati iliyoandikwa ya kutushitaki” (Wakolosai 2:14). Wazo hili limerudiwa zaidi ya mara moja katika Agano Jipya: “Mtu mmoja afanya tofauti kati ya siku na siku; mwinginie aona siku zote kuwa sawasawa. Kila mtu na athibitike katika akili zake mwenyewe. Yeye aadhimishaye siku huiadhimisha kwa Bwana” (Warumi 14:5-6a). “Bali sasa mkiisha kumjua Mungu, au zaidi kujulikana na Mungu, kwa nini kuyarejea tena mafundisho ya kwanza yaliyo manyonge, yenye upungufu, ambayo mnataka kuyatumikia tena? Mnashika siku, na miezi, na nyaktati, na miaka” (Wagalatia 4:9-10). Bali wengine wanadai kuwa agizo la Constantino katika mwaka wa 321 A.D (Baada ya Yesu kuzaliwa) ilibadilisha sabato kutoka Jumamosi hadi Jumapili. Ni siku gani kanisa la kwanza lilikutana kwa ibada? Bibilia haitaji mkusanyiko wowote wa sabato (Jumamosi) kwa waumini kwa minajili ya ushirika au ibada. Ingawa, kuna kurasa wazi zinazoitaja siku ya kwanza ya juma. Kwa mfano Matendo Ya Mitume 20:7 ambayo yasema, “Hata siku ya kwanza ya juma, tulipokutana ili kumega mkate.” Katika 1 Wakorintho 16:2 Paulo anawasihi Wakristo wa Korintho, “Siku ya kwanza ya juma kila mtu kwenu na aweke akiba kwake, kwa kadri ya kufanikiwa kwake.” Jinsi Paulo anayataja haya matoleo kuwa “huduma” katika 2 Wakorintho 9:12, haya matoleo lazima yamehuzishwa na ibada ya siku ya Jumapili ya Wakristo. Kiistoria siku ya Jumapili, bali si Jumamosi ilikuwa siku iliyokubalika kwa Wakristo katika kanisa na matukio yao yaweza kufuatwa hadi wakati wa kanisa la kwanza. Sabato ilipeanwa kwa Waisraeli, si kanisa. Sabato bado ingali siku ya Jumamosi si Jumapili na haijawai badilishwa. Bali sabato ni sehemu ya sheria ya Agano La Kale na Wakristo wako huru kutoka kwa mkono wa sheria (Wagalatia 4:1-26; Warumi 6:14). Wakristo hawitakiwi kuitunza sabato hata kama iko siku ya Jumamosi au Jumapili. Siku ya kwanza ya juma, siku ya Bwana (Ufunuo 1:10) za sherekea kiumbe kipya Kristo aliyefufuka akiwa kiongozi wetu. Hatujaamrishwa kiufuata sheria ya Musa ya sabato ya kustarehe, bali tuko huru kumfuata Kristo aliyefufuka. Mtume Paulo alisema kwamba kila mkristo amue mweneyewe kama ataifuata sabato, “Mtu mmoja afanya tofauti kati ya siku na siku; mwingine aona siku zote kuwa sawasawa. Kila mtu na athibitike katika akili zake mwenyewe” (Warumi 14:5). Twastahili kumwabudu Mungu kila siku, si Jumamosi pekee or Jumapili pekee.

Makundi mawili ya watu katika maisha yako.

FAHAMU MAKUNDI MAWILI YA WATU KATIKA MAISHA YAKO.
Na Steven Mshiu.
Maisha ya kila mwanadamu yamezungukwa na watu. Watu hawa waweza katika makundi mbalimbali. Waweza kuwa watu wema au wabaya. Hali na vipato vyetu husababisha kutokea mgawanyiko na kutengeneza makundi. Leo nataka nikupe aina mbili za makundi haya.

KUNDI LA KWANZA: KUTOKA NDANI KWENDA NJE:
Hili ni kundi ambalo lipo pamoja na wewe. Nia ya kundi hili sio nzuri hata kidogo. Lipo na wewe pale unapokuwa katika raha tu. Watakula na kunywa vyako. Watatumia kila kilicho chako. Hii ni kwa sababu una kitu. Siku ukiishiwa Kundi hili hutoka upande wako, kwenda nje ya maisha yako.

Halikuthamini tena kwa sababu umefikwa na upungufu. Siku zote hubeba taarifa zako mbaya na kuzipeleka nje. Kama huna akili ya ziada huwezi kulitambua kundi hili hadi pale utakapofikwa na tatizo ndipo utakapofahamu uhalisia wa kundi hili.

KUNDI LA PILI:KUTOKA NJE KUJA NDANI
Hili ni kundi ambalo mara nyingi huwezi kulipa thamani yake. Halipo na wewe pale unapokuwa katika raha au furaha. Pale unapofikwa na matatizo ndipo linapojitokeza. Kundi hili hubeba habari za matumaini. Hubeba habari ya kurejeshwa tena. Hubeba habari za kutia moyo.
Kundi hili hutoka nje na kuja kwako.

Wakati lile kundi la kwanza likitoka kwako kwenda nje na hili la pili linalotoka nje kuja kwako lile kundi la kwanza hujaribu kulivunja moyo lile kundi la pili kwamba mambo yameharibika, Hivyo lisijisumbue kuja kwako. Lakini kwa sababu kundi hili la pili limebeba habari za matumaini huwa halivunjiki moyo.

Luka 8:49-56, Hapa tunaona makundi mawili, moja ni la Yesu lakini la pili ni la waombolezaji. Kundi la Yesu linaletewa habari ya msiba wa binti, Yesu anasema kuwa yule binti hajafa kwani amelala tu, Lakini lile kundi lingine linazipinga habari au taarifa za matumaini zilizotolewa na Yesu za urejesho wa uhai wa binti yule.

Kundi hili lipo pamoja na mfiwa likiomboleza na kulia lakini pale linaposikia habari za binti kurejeshewa uhai linaanza kucheka na kulibeza lile kundi lililotoa habari za matumaini.
Ndivyo ilivyo hata katika maisha yetu, Kuna kundi utaliona lipo pamoja na wewe lakini nia yake ni kukuona tu ukiwa katika hali mbaya. Halipendi kukuona ukiwa umefanikiwa. Halipendi kukuona ukipata kitu. Kupoteza kwako kwao ni furaha. Cha ajabu laweza kuwa ni kundi la wapendwa. Liepuke kundi hili.

Usifikiri kila mtu ni mwema kwako. Kuna ambao wanalia pamoja na wewe lakini mioyoni wao wanacheka. Kuna wanaokutia moyo lakini dhamira zao zinawashughudia kabisa kuwa ni wanafiki. Kuna ambao kwa nje wanaonyesha nyuso za furaha na kufurahi pamoja pale unapokuwa umepata kitu, Lakini mioyoni mwao wana huzuni kuu, kwanini wewe umepata.

Mpendwa rafiki jitahidi ukae upande wa kundi hili la pili. Hili ni kundi lenye habari za mafanikio, Hubeba habari njema. Kundi hili hutokea na kuchukua nafasi inayoachwa na kundi la kwanza.
Mungu akusaidie kuyapambanua makundi ya watu wanaokuzunguka.

Steven Mshiu
0655 882074
Thursday, 16Nov2017

Jumatatu, 13 Novemba 2017

TAFUTA KUTETEWA NA MUNGU TU.

TAFUTA KUTETEWA NA MUNGU TU.

Na Steven Mshiu

Natamani nimtie moyo mtu mmoja ambaye anaona amekwama na kila akiangalia mbele haoni mpenyo. Kila kona amezungukwa na maadui, watu wanakunenea mambo ya ajabu.

Unaishi kwa wasiwasi kutokana na vitisho vya adui zako. Umekata tamaa kabisa kwa kuwa huoni msaada wowote.

NISIKILIZE.

Mfalme Senakerbu aliyekuwa akiitawala Ashuru ambayo kwa sasa ni Siria, aliinuka na kuanza kuipiga baadhi ya miji ya Yuda kisha akaitwaa. Mfalme huyu wa Ashuru au Siria hakuwa anamfahamu Mungu kabisa.
Aliabudu miungu, na inasemekana kwamba miji hii aliyofanikiwa kuiteka nayo pia walikuwa ni waabudu miungu ambayo ni kazi za mikono ya wanadamu.
Baada ya kufanikiwa kuiteka miji hii akadhamiria kuiteka Yerusalemu ya Israel iliyokuwa ikitawaliwa na Mfalme Hezekia.

Historia ya Hezekia kwa kifupi ni kwamba alikuwa ni miongoni mwa wafalme waliokuwa wakimfahamu MUNGU wa kweli. Kila alichokifanya alitegemea msaada wa MUNGU, Hakufanya chochote kile bila kumuuliza Mungu. Kwa ufupi alimtetea na kumdhihirisha Mungu wake, kuwa ni MUNGU WA MSAADA.

Huyu Senakerbu akatuma waraka kwa taifa la Israel ili kuwavunja moyo, kuwa Hezekia anawadanganya kuwa huyo Mungu wake hawezi kuwatetea, hivyo mje kwangu ili muwe watu wangu, maana yake taifa la Israel liwe watumwa kwa Ashuru chini ya mfalme Senakerbu.
Hiki kilikuwa ni kipindi kigumu sana kwa Hezekia kutokana na Senakerbu kuwa na nguvu kubwa sana ya kijeshi. Hezekia hakuona popote pale ambapo angeweza kupata msaada. Baada ya kupata ule Biblia inaniambia kuwa Hezekia alirarua mavazi yake ya kifalme akavaa magunia na kuanza kumtafuta Mungu wake.

Alitambua kuwa hakuna mtetezi mwingine zaidi yake. Mfalme akaingia magotini kumwomba MUNGU. Ona maombi yake katika Isaya 37:15-20, moja kwa moja tunaona ni namna gani mfalme huyu alivyokuwa akimtetea Mungu wake.

Mungu anapenda kutetewa, anampenda mtu aliye tayari kujitoa kwa ajili yake. Niweke sawa jambo moja, Ninaposema kuwa Mungu anapenda kutetewa simaanishi kwamba yeye ameshindwa kujitetea mwenyewe. La Hasha. Anatamani aone mwanadamu anaweza kusimama upande wake kwa kiasi gani.

Mungu alimuumba mwanadamu kwa ajili ya utukufu wake. Hivyo mwanadamu anapofurahia kazi ya muumbaji wake na kuwa na wivu naye Mungu hujisikia vizuri sana, Kule kumtetea Mungu humfanya ashindwe kutulia katika kiti chake cha Enzi hivyo hushuka na kututetea sisi pale tunapokuwa tumeshindwa.

Kutokana na ujasiri huu wa Hezekia kumtetea Mungu wake, Katika sura ya 37: kuanzia mstari wa 21, Mungu anajibu au anajitokeza ili kumtetea Hezekia. Kwa kifupi ni kwamba hapa Hezekia aliuza kesi yake kwa Mungu. Hivi unafikiri Mungu atamfanya nini huyu Senakerbu? Kwanza alitukana Mungu, Akamtisha Mtu anaemtegemea Mungu. Akamuona Mungu kama ni vile vimiungu alivyoviharibu ambavyo vilitengenezwa kwa mikono ya wanadamu.

Kuanzia mstari wa 29, Mungu anaanza kusema vile atakavyomtenda huyu Senakerbu, kwanza atamfunga pua na huo mdomo unaomtukana Mungu, Ukizibwa pua na mdomo sidhani kama unaweza kuishi kwa zaidi ya dakika kumi. Lakini pia hataweza kutimiza azma yake ya kuiteka Yerusalemu kwani Mungu anasema atamrudisha kwa njia ile ile aliyoijia.
Mungu akamtoa Hezekia wasiwasi na kumhakikishia kuwa ATAMTETEA na ataulinda ule mji na kuuokoa. vs 35

Kilichomkuta Senakerbu sio kizuri, Isaya 37:36, watu wanaamka asubuhi zaidi ya watu laki na themanini wamekufa haijulikani waliuawa na nani , Senakerbu naye akiwa anaabudu miungu yake(Niskori) wanawe walimtokea na kumuua kwa upanga.
Hali ikawa shwari kwa Hezekia.

Inawezekana hata kwako maadui zako wameinuka kwa ajili yako hebu mwombe MUNGU akutete.
Yale ambayo unayaona ni mazito kwako kila ukiwaza unaona hakuna njia kabisa Biblia inasema katika Zaburi 37:1-7 MKABIDHI BWANA NJIA ZAKO na MAWAZO YAKO YATATHIBITIKA
pia anasema ni jambo gani ambalo yeye hawezi. Hapana. Anaweza kila jambo,

Mathayo 11:28-29, Anasema kuwa Mizigo yetu tumtwike yeye(YESU) kwani nira yake ni laini na mzigo wake ni mwepesi. Yeye peke yake ndiye mtetezi anayeza kuleta furaha na raha ya nafsi. Huyu ndiye aliyemletea Hezekia furaha ya nafsi yake. Hata wewe anaweza kukuletea raha ya nafsi yako.

Lile unaloliona ni gumu lisukumize kwa Mungu, Hakika yeye ndiye mtetezi wa haki. Wanadamu wanaweza kukutetea lakini watakudai uwalipe, Lakini Mungu ndiye MTETEZI pekee asiyetaka malipo zaidi ya kumsifu na kurudisha sifa na utukufu kwake.

Ubarikiwe sana mtu wa Mungu. Inuka. Sio wakati wa kukaa tena chini. Sio wakati wa kusononeka tena. Tafuta kutetewa na Mungu..

Tafuta kuipata RAHA ya nafsi yako.
Nikutie moyo kuwa "BWANA ATAKUPIGANIA NAWE UTANYAMAZA KIMYA"

Steven Mshiu
0655-882074
Nov 13, 2017.

Ijumaa, 10 Novemba 2017

JIFUNZE KWA TAI

LENGO LA JARIBU SIO KUKUUMIZA.

Na Steven Mshiu

Nimefika ofisini mapema leo hii asubuhi. nikaukumbuka wimbo wa Ambwene unaosema "TANGULIA MBELE". Nimetumia zaidi ya nusu saa kuusikiliza huku nikitafakari mambo mengi sana.

Kwenye wimbo huu amemzungumzia ndege aina ya TAI.
Tai ni miongoni mwa ndege wakubwa sana tena wa ajabu. Mazingira ambayo Tai wanaishi ni tofauti kabisa na mazingira wanayoishi ndege wengine.

Tai hujenga kiota chake mahali ambapo hakuna chochote kile kinachoweza kumdhuru kufika. Hujenga kwenye maporomoko makali sana. Ni vigumu sana kwa nyoka na hatari nyingine kufikia kiota hicho.

Tai ni ndege anaeweza kuruka juu sana kuliko ndege wengine. Ni ndege aliyebarikiwa hekima na busara nyingi sana.

Lengo la Tai kufanya hivyo ni kuhakikisha usalama wa uzao wake.
Wakati anapojenga kiota chake, hutanguliza miiba mikali halafu kwa juu huifunika ile miiba kwa manyoya yake, Hivyo yale makinda yake yanapokaa pale kwenye kiota hufurahia sana joto la yale manyoya na hayafahamu kama kuna miiba kwa chini,

Mama yao hufanya juhudi kubwa sana kuyatafutia chakula, na pale anapokosa hujitoa manyoya upande wa chini wa tumbo lake hivyo anapokuja kukaa karibu na makinda yake huanza kula nyama kutoka kwenye mwili wa TAI huyo,

Kadri siku zinavyokwenda yale makinda hupata nguvu. Hufikia wakati yakajitafutie chakula. Mama huanza mafunzo rasmi. Kwanza huyanyima chakula ili yatoke pale kwenye kiota. Yanapokataa kutoka mama yao huyapuliza yale manyoya hivyo ile miiba huanza kuyachoma yale makinda.

Huanza kutoka bila kupenda. Mama yao huyachukua hadi juu sana halafu huyaachia. Yale makinda yanaporuka huruka bila muelekeo. Huweza kuhisi kama mama yao anawachukia. Yanapofikia hatua ya kuishiwa nguvu, Mama yao hutokeza kwa mbele na kuyanyaka.
Hapo ndipo hugundua hekima na upendo wa mama yao

 TUNAJIFUNZA NINI KUHUSU TAI??

Mungu kwetu yeye ni kama TAI, sisi ni makinda yake. Aliandaa mazingira mazuri sana kwa ajili yetu sisi kuishi. Lakini alifahamu kuwa humu duniani kuna majaribu ya kila aina. Na mpango wake sio tuangamie kenye majaribu hayo.

Anasema hakuna jaribu linalompata mtu linalozidi uwezo wake.
Lengo la majaribu hayo ni kutupa mafunzo ya kuweza kuimarika katika imani ili tuendelee kumtegemea yeye.

Mara nyingi tunaweza kuishi bila kutambua kuwa kuna changamoto au majaribu, Hii ni kwa sababu ya neema ya kipekee ya Mungu. Unaweza kuishi bila kujua njaa ni nini. Unaweza kuishi bila kujua shida ni nini?

Hivyo Mungu huondoa ile neema ili utambue kuwa yeye ni nani na ufahamu upendo wake kwetu ukoje. Kama vile Tai anapoyanyima makinda yake chakula ndivyo ilivyo Mungu wetu aanapotupitisha kwenye jaribu. Pale unapoleta kiburi huondoa kile kitu ambacho kinakupa kiburi hivyo hukulazimu kutoka tuu.

TAI huyapuliza yale mmanyoya hivyo yale makinda hutoka pale kiotani tu.
Mungu anataka tutoke, tukalitimize kusudi lake. Lakini sisi tumeng'ang'ania kwenye kiota tu. Tulipookoka tu tulilibeba kusudi la Mungu la kuufikia Ulimwengu. Pale tunapofika kanisani tunajiona kama tumefika. Hapana tunatakiwa kutoka.

Akili zetu haziwezi kukua kama tutaendelea kubaki kwenye kiota. Tutaendelea kulishwa tu. Ifike mahali nasi tutosheke kulishwa nasi tukalishe.

Hivyo mpango wa Mungu kutupitisha kwenye majaribu, mwanzoni tunaweza kuona kama Mungu anatuonea lakini pale tunapoanza kupita katika jaribu hilo na tukaonyesha kumhitaji yeye, yeye hutupa nguvu za kustahimili jaribu jaribu hilo

Na hatimaye hutuinua na kutuweka katika viwango vingine.

Nikukumbushe jambo moja la muhimu. CHANGAMOTO sio zakukuumiza bali ni za KUKUIMARISHA.
Steven Mshiu
Nov 10, 2017

Ijumaa, 27 Oktoba 2017

MUNGU HAJAKUSAHAU..

JAPO WATAKUSAHAU, MUNGU ANAKUKUMBUKA.

Na Steven Mshiu

Mara nyingi sisi kama wanadamu tumekuwa tukifikia hatua ya kuona tumesahaulika kabisa. Hali hii hasa hutokea pale tunapokuwa tumeingia katika shida au matatizo, aidha ugonjwa, mkwamo wa maisha na mambo mengine mengi tu,

Nilimsikia mtu mmoja aliyekuwa mgonjwa akilalamika sana kuwa ndugu zake hawajaenda kumwona pale hospitali, akafikia hatua hata ya kulaani kabisa. Kwake kutotembelewa na ndugu zake kwa siku chache tu alijiona kama wamemshau na hawampendi kabisa.
Lakini pia ni kawaida ya wanadamu kumkimbia au kumtenga mtu aliyeingia kwenye shida fulani. Mtu huyo anaweza kuwa katika hali ya upweke mkubwa, kukata tamaa, kukosa tumaini maana hana mtu wa kumfariji.

Kipindi Yesu akiwa pale msalabani alikutana na hali hii, alihisi upweke mkubwa sana. Aliangalia wale aliowapa mikate na kuwaponya ndio hao hao wanamsulubisha. Wale aliokuja kuwaletea wokovu ndio hao hao wanamsulubisha. Akafikia hatua ya kumlaumu Mungu kuwa mbona amemuacha? Lakini sio kweli kwamba Mungu alikuwa amemuacha au amemsahau.

Yusufu aliyekuwa na ndoto kubwa lakini akaangukia gerezani akiwa pamoja na wafungwa wenzake, hawakutengwa na yale matatizo yao. Lakini pale tu kulipotokea mpenyo baadhi ya wafungwa wakatoka mle gerezani. Yusufu alijihisi upweke na kuona wale wafungwa wenzake waliokuwa pamoja mle gerezani wamemsahau.

Japo wafungwa hawa waliweza kumsahau Yusufu sio kwamba Mungu alikuwa amemsahau Yusufu. La hasha. Bado kile Mungu alichokisema kwa Yusufu Ni lazima kitimie tu, Ni kiasi cha muda na wakati tuu uwadie.

Nataka nikukumbushe kitu kimoja kuwa. Mungu ni mwaminifu na ni Mungu wa maagano. Kile alichokisema juu ya maisha yako unaweza kuona kama anachelewa au amekusahau, lakini atakitimiza kwa wakati wake tuu.

Mwanadamu anaweza akakuahidi kitu lakini akasahau. Kipindi fulani tulikuwa tukijiandaa na sherehe ya kumuaga dada yetu(send Off) mtu mmoja aliniahidi mchango, lakini akasahau hivyo hakunipatia mchango ule. Lakini Mungu wetu akiahidi kukubariki ni lazima atakubariki tu.

Wakati wa Mungu kukumbuka ukifika kila mtu atashangaa, Hata wewe mwenyewe utajishangaa. Kibinadamu ni ngumu sana kutoka gerezani na kuwa waziri mkuu kwa wakati huo. Lakini hilo liliwezekana kwa Yusufu maana Mungu alimkumbuka.

Waweza kudhani Mungu amekusahau kila ukipata mchumba baada ya muda mfupi mchumba anayeyuka kama mshumaa, Mungu aliyemkumbuka Hana na Sara atakukumbuka na wewe.
Waweza kudhani kuwa Mungu amekusahau kwenye ajira vyeti vizuri unavyo, elimu nzuri unayo, Mungu aliyemkumbuka Daniel na wenzake atakukumbuka na wewe.

Umeolewa lakini unashuhudia wenzako wakiwapeleka watoto wao kliniki lakini kwako huu ni mwaka wa sita sasa, unahisi Mungu amekusahau. Mapema sana Mungu atakukumbuka kwa kukuletea Isaka.

Jambo moja la kuzingatia:
Usikubali kuchukua maamuzi yoyote yanayokujia kwenye akili yako pindi unapokuwa katika msongo wa mawazo ya kuhisi kuwa Mungu amekusahau. Sara aliamua kuchukua uamuzi wa kumshauri Ibrahimu azae na kijakazi wake Hajiri. Haya hayakuwa maamuzi sahihi kwa Sara.

Jifunze kumngoja Mungu,
Jifunze kuziamini ahadi zake.
Ongeza kiwango chako cha Subira.

Maamuzi ya Sara ni tofauti kabisa na maamuzi ya Hana.

Kumbuka wote hawa walipitia kwenye shida zinazofanana.
Usikubali shida au jaribu lako likutoe kwenye viwango vyako vya kumwamini Mungu.
 
Pia usisahau kumshukuru Mungu kwa chochote kile anachokutendea. Jitahidi kulipa fadhila hata kwa wale uliowaona kuwa wamekusahau pindi Mungu atakapokukumbuka.

Steven Mshiu
0655 882074
0768 882074
Fr. Oct 27, 2017

Jumatatu, 23 Oktoba 2017

HAKIKISHA UNAMALIZIA VIZURI

UKIANZA VIZURI HAKIKISHA UNAMALIZIA VIZURI.
Na Steven Mshiu,
Shalom mtu wa Mungu. Ninamtukuza yeye kwa kunijaalia pumzi ambayo siilipii hata senti moja. Hii ni neema ya kipekee ambayo nimepewa na Mungu. Naamini hata kwako umepewa neema hii.

Nikupe hongera na pole kwa mikiki mikiki ya kupambana na maisha haya ambayo kila kunapokucha yanakabiliwa na changamoto mbalimbali. Lakini kwa sababu tupo hapa duniani kwa kusudi maalumu ni dhahiri kuwa tutafikia mwisho mwema.

Nirudi kwenye kile ambacho nilitaka tukumbushane siku ya leo. Kama nilivyoanza kwa kichwa chenye maneno haya kuwa “UKIANZA VIZURI HAKIKISHA UNAMALIZIA VIZURI”, ina maana unaweza ukaanza vizuri na ukamalizia vibaya au ukaanza vibaya na ukamalizia vizuri au ukaanza vibaya na ukamalizia vibaya.

Jambo moja la msingi na la muhimu ni kujiuliza kuwa umeridhika na huo mwisho wako? Mwisho wako umekuletea matokeo chanya?. Kama umekuletea umekuletea matokeo chanya basi hongera, na kama umekuletea matokeo hasi ni wakati wa kukaa chini na kujitafakari ni wapi ambapo ulifanya vibaya ili uweze kuchukua NAFASI NYINGINE ya kufanya vizuri zaidi.

Leo kuna watu wanaanza mahusiano yao katika hali ya utakatifu. Ukiuangalia mwanzo wao unajisemea moyoni hawa watu ni lazima watafika mbali tu, lakini kadri siku zinavyokwenda ule utakatifu wa mwanzo unaanza kupungua kidogo kidogo. Ile nidhamu binafsi inapungua kidogo kidogo. Walikuwa na lengo la kufunga ndoa takatifu, mwezi mmoja kabla ya ndoa wanaanguka katika dhambi ya uzinzi.

Mwingine alianza safari yake ya wokovu, safari yenye uhakika wa kufika mbinguni, alihudhuria vipindi vyote kanisani, hakukosa ibaada hata siku moja, alikuwa mwaminifu kwa Mungu, lakini kadri muda unavyokwenda dunia na anasa zake zikaanza kumzuzua. Fasheni za dunia zikamponza, marafiki wakamponza, ile hali ya kumpenda Mungu ikaanza kuporomoka, mwishowe akamwacha Mungu kabisa. Mara nyingi pale tunaporidhika na mwanzo wetu na kujihakikishia kuwa hauhitaji kuboreshwa zaidi ndipo tunapoanza kuharibu na kutengeneza mwisho mbaya.

Yesu akasema kuwa ile saa tusiyodhani ndiyo saa ambayo mwana wa ADAM atakaporudi. Wengi tutakuwa hatujauandaa mwisho wetu maana tulishabweteka na mwanzo wetu.

Mpendwa hakikisha mwisho wako unakuwa ni mwema.
Isije ikawa tumeumia kuutengeneza mwanzo wetu halafu tukausahau mwisho wetu. Hivi ni vitu viwili vya muhimu vya kuangalia na kuzingatia.

Tunaposoma Biblia, leo nimekutana na kisa hiki cha mfalme Yosia, mwana wa Amoni, mwana wa Manase. Yosia alianza kutawala Yerusalemu akiwa na miaka nane. Kabla ya hapo alitanguliwa na baba yake alieitwa Amoni ambaye alifanya machukizo mengi mbele za Mungu kama alivyofanya baba yake Manase.

Wafalme hawa waliiacha njia ya Mungu wakaiandama miungu na ibaada za sanamu. Alipoingia ktk ufalme kinda huyu wa Amoni, baada ya babaye Amoni kuuawa, YOSIA hakutaka kuifuata njia ya wazazi wake. Akaamua kumuelekea Mungu, akadhamiria kumtafuta Mungu. Akaanza kuisafisha nyumba ya MUNGU ambayo ilitelekezwa kwa muda mrefu, akazivunja ashera zote na madhabahu zote za miungu ya wazazi wake.

Kwa ufupi alifanya matengenezo makubwa kati ya Mungu na wana wa Israel. Tunaweza kusema kuwa alifanya huduma ya utakaso. Ule upako na uwepo wa Mungu ukarudi tena juu ya Israel maana MUNGU alishakasirishwa na uovu wa MANASE na AMON. Yosia akawa amefanikiwa kwa kiasi kikubwa sana katika ufalme wake.

Na kwa kuwa mfalme huyu alienza kutawala akiwa na umri mdogo sana, alianza vizuri na Mungu wake, Mungu alimstarehesha sana, hakuna sehemu inayosema kuwa kuna maadui walioinuka ili wapigane na ufalme wake. Biblia inasema katika 2 Wafalme 23:25, Kabla ya huyo hapakuwa na mfalme mfano wake aliemwelekea BWANA Kwa moyo wake wote na kwa roho yake yote na kwa nguvu zake zote sawasawa na sheria zote za Musa wala baada yake hakuinuka mmoja mfano wake yeye.

Ni kweli kabisa anahitaji kupongezwa.
Sasa je mwisho wake unakuwaje?
Baada ya Mungu kumneemesha mfalme huyu, kumstarehesha kila pande, akaamua kujitia kiherehere cha kuingilia vita isiyomhusu. Ukisoma katika 2 Wafalme 23:29, Farao-neko mfalme wa Misri anainuka kupigana na mfalme wa Ashuru, haya ni mataifa mawili tofauti kabisa na israel/Yerusalemu,. Lakini Yosia akaenda ili apigane. Huyu mfalme wa Misri akamuua Yosia.
Huo ukawa mwisho wa kizembe kabisa wa mfalme Yosia ambae alianza vizuri hadi kusifiwa na Mungu.

Mpendwa mtu wa Mungu kuna mambo mengi sana kujifunza hapa:
1. Ni mambo mangapi tulianza vizuri lakini kadri siku zinavyokwenda tunatengeneza mwisho mbaya?
2. Je pale tunapogundua kuwa mwisho wetu unakuwa mbaya ni hatua gani za kuchukua?
3. Je tunabweteka na mwanzo wetu, na kujihalalishia kuwa sisi tumeshakamilika hivyo tuna uwezo wa kujiongoza wenyewe?
4. Je tuko tayari kuyaacha yale yote yanayosababisha mwisho wetu kuwa mbaya?
5. Je tunatambua kuwa Mungu anafahamu mwanzo wetu na mwisho wetu, ila ametupa "option" ya kuchagua tuanzeje na tumalizieje?
Mungu akubariki sana.
Nakutakia tafakari njema
#USIISHIE_NJIANI
Imeandikwa na
Steven Mshiu,
0655-882074
au baruapepe smshiu42@gmail.com
Oct 20, 2017

MAKUNDI MAWILI YA WATU WANAOKUZUNGUKA.

FAHAMU MAKUNDI MAWILI YA WATU KATIKA MAISHA YAKO. Na Steven Mshiu . Maisha ya kila mwanadamu yamezungukwa na watu. Watu hawa waweza kat...