Ijumaa, 27 Oktoba 2017

MUNGU HAJAKUSAHAU..

JAPO WATAKUSAHAU, MUNGU ANAKUKUMBUKA.

Na Steven Mshiu

Mara nyingi sisi kama wanadamu tumekuwa tukifikia hatua ya kuona tumesahaulika kabisa. Hali hii hasa hutokea pale tunapokuwa tumeingia katika shida au matatizo, aidha ugonjwa, mkwamo wa maisha na mambo mengine mengi tu,

Nilimsikia mtu mmoja aliyekuwa mgonjwa akilalamika sana kuwa ndugu zake hawajaenda kumwona pale hospitali, akafikia hatua hata ya kulaani kabisa. Kwake kutotembelewa na ndugu zake kwa siku chache tu alijiona kama wamemshau na hawampendi kabisa.
Lakini pia ni kawaida ya wanadamu kumkimbia au kumtenga mtu aliyeingia kwenye shida fulani. Mtu huyo anaweza kuwa katika hali ya upweke mkubwa, kukata tamaa, kukosa tumaini maana hana mtu wa kumfariji.

Kipindi Yesu akiwa pale msalabani alikutana na hali hii, alihisi upweke mkubwa sana. Aliangalia wale aliowapa mikate na kuwaponya ndio hao hao wanamsulubisha. Wale aliokuja kuwaletea wokovu ndio hao hao wanamsulubisha. Akafikia hatua ya kumlaumu Mungu kuwa mbona amemuacha? Lakini sio kweli kwamba Mungu alikuwa amemuacha au amemsahau.

Yusufu aliyekuwa na ndoto kubwa lakini akaangukia gerezani akiwa pamoja na wafungwa wenzake, hawakutengwa na yale matatizo yao. Lakini pale tu kulipotokea mpenyo baadhi ya wafungwa wakatoka mle gerezani. Yusufu alijihisi upweke na kuona wale wafungwa wenzake waliokuwa pamoja mle gerezani wamemsahau.

Japo wafungwa hawa waliweza kumsahau Yusufu sio kwamba Mungu alikuwa amemsahau Yusufu. La hasha. Bado kile Mungu alichokisema kwa Yusufu Ni lazima kitimie tu, Ni kiasi cha muda na wakati tuu uwadie.

Nataka nikukumbushe kitu kimoja kuwa. Mungu ni mwaminifu na ni Mungu wa maagano. Kile alichokisema juu ya maisha yako unaweza kuona kama anachelewa au amekusahau, lakini atakitimiza kwa wakati wake tuu.

Mwanadamu anaweza akakuahidi kitu lakini akasahau. Kipindi fulani tulikuwa tukijiandaa na sherehe ya kumuaga dada yetu(send Off) mtu mmoja aliniahidi mchango, lakini akasahau hivyo hakunipatia mchango ule. Lakini Mungu wetu akiahidi kukubariki ni lazima atakubariki tu.

Wakati wa Mungu kukumbuka ukifika kila mtu atashangaa, Hata wewe mwenyewe utajishangaa. Kibinadamu ni ngumu sana kutoka gerezani na kuwa waziri mkuu kwa wakati huo. Lakini hilo liliwezekana kwa Yusufu maana Mungu alimkumbuka.

Waweza kudhani Mungu amekusahau kila ukipata mchumba baada ya muda mfupi mchumba anayeyuka kama mshumaa, Mungu aliyemkumbuka Hana na Sara atakukumbuka na wewe.
Waweza kudhani kuwa Mungu amekusahau kwenye ajira vyeti vizuri unavyo, elimu nzuri unayo, Mungu aliyemkumbuka Daniel na wenzake atakukumbuka na wewe.

Umeolewa lakini unashuhudia wenzako wakiwapeleka watoto wao kliniki lakini kwako huu ni mwaka wa sita sasa, unahisi Mungu amekusahau. Mapema sana Mungu atakukumbuka kwa kukuletea Isaka.

Jambo moja la kuzingatia:
Usikubali kuchukua maamuzi yoyote yanayokujia kwenye akili yako pindi unapokuwa katika msongo wa mawazo ya kuhisi kuwa Mungu amekusahau. Sara aliamua kuchukua uamuzi wa kumshauri Ibrahimu azae na kijakazi wake Hajiri. Haya hayakuwa maamuzi sahihi kwa Sara.

Jifunze kumngoja Mungu,
Jifunze kuziamini ahadi zake.
Ongeza kiwango chako cha Subira.

Maamuzi ya Sara ni tofauti kabisa na maamuzi ya Hana.

Kumbuka wote hawa walipitia kwenye shida zinazofanana.
Usikubali shida au jaribu lako likutoe kwenye viwango vyako vya kumwamini Mungu.
 
Pia usisahau kumshukuru Mungu kwa chochote kile anachokutendea. Jitahidi kulipa fadhila hata kwa wale uliowaona kuwa wamekusahau pindi Mungu atakapokukumbuka.

Steven Mshiu
0655 882074
0768 882074
Fr. Oct 27, 2017

Jumatatu, 23 Oktoba 2017

HAKIKISHA UNAMALIZIA VIZURI

UKIANZA VIZURI HAKIKISHA UNAMALIZIA VIZURI.
Na Steven Mshiu,
Shalom mtu wa Mungu. Ninamtukuza yeye kwa kunijaalia pumzi ambayo siilipii hata senti moja. Hii ni neema ya kipekee ambayo nimepewa na Mungu. Naamini hata kwako umepewa neema hii.

Nikupe hongera na pole kwa mikiki mikiki ya kupambana na maisha haya ambayo kila kunapokucha yanakabiliwa na changamoto mbalimbali. Lakini kwa sababu tupo hapa duniani kwa kusudi maalumu ni dhahiri kuwa tutafikia mwisho mwema.

Nirudi kwenye kile ambacho nilitaka tukumbushane siku ya leo. Kama nilivyoanza kwa kichwa chenye maneno haya kuwa “UKIANZA VIZURI HAKIKISHA UNAMALIZIA VIZURI”, ina maana unaweza ukaanza vizuri na ukamalizia vibaya au ukaanza vibaya na ukamalizia vizuri au ukaanza vibaya na ukamalizia vibaya.

Jambo moja la msingi na la muhimu ni kujiuliza kuwa umeridhika na huo mwisho wako? Mwisho wako umekuletea matokeo chanya?. Kama umekuletea umekuletea matokeo chanya basi hongera, na kama umekuletea matokeo hasi ni wakati wa kukaa chini na kujitafakari ni wapi ambapo ulifanya vibaya ili uweze kuchukua NAFASI NYINGINE ya kufanya vizuri zaidi.

Leo kuna watu wanaanza mahusiano yao katika hali ya utakatifu. Ukiuangalia mwanzo wao unajisemea moyoni hawa watu ni lazima watafika mbali tu, lakini kadri siku zinavyokwenda ule utakatifu wa mwanzo unaanza kupungua kidogo kidogo. Ile nidhamu binafsi inapungua kidogo kidogo. Walikuwa na lengo la kufunga ndoa takatifu, mwezi mmoja kabla ya ndoa wanaanguka katika dhambi ya uzinzi.

Mwingine alianza safari yake ya wokovu, safari yenye uhakika wa kufika mbinguni, alihudhuria vipindi vyote kanisani, hakukosa ibaada hata siku moja, alikuwa mwaminifu kwa Mungu, lakini kadri muda unavyokwenda dunia na anasa zake zikaanza kumzuzua. Fasheni za dunia zikamponza, marafiki wakamponza, ile hali ya kumpenda Mungu ikaanza kuporomoka, mwishowe akamwacha Mungu kabisa. Mara nyingi pale tunaporidhika na mwanzo wetu na kujihakikishia kuwa hauhitaji kuboreshwa zaidi ndipo tunapoanza kuharibu na kutengeneza mwisho mbaya.

Yesu akasema kuwa ile saa tusiyodhani ndiyo saa ambayo mwana wa ADAM atakaporudi. Wengi tutakuwa hatujauandaa mwisho wetu maana tulishabweteka na mwanzo wetu.

Mpendwa hakikisha mwisho wako unakuwa ni mwema.
Isije ikawa tumeumia kuutengeneza mwanzo wetu halafu tukausahau mwisho wetu. Hivi ni vitu viwili vya muhimu vya kuangalia na kuzingatia.

Tunaposoma Biblia, leo nimekutana na kisa hiki cha mfalme Yosia, mwana wa Amoni, mwana wa Manase. Yosia alianza kutawala Yerusalemu akiwa na miaka nane. Kabla ya hapo alitanguliwa na baba yake alieitwa Amoni ambaye alifanya machukizo mengi mbele za Mungu kama alivyofanya baba yake Manase.

Wafalme hawa waliiacha njia ya Mungu wakaiandama miungu na ibaada za sanamu. Alipoingia ktk ufalme kinda huyu wa Amoni, baada ya babaye Amoni kuuawa, YOSIA hakutaka kuifuata njia ya wazazi wake. Akaamua kumuelekea Mungu, akadhamiria kumtafuta Mungu. Akaanza kuisafisha nyumba ya MUNGU ambayo ilitelekezwa kwa muda mrefu, akazivunja ashera zote na madhabahu zote za miungu ya wazazi wake.

Kwa ufupi alifanya matengenezo makubwa kati ya Mungu na wana wa Israel. Tunaweza kusema kuwa alifanya huduma ya utakaso. Ule upako na uwepo wa Mungu ukarudi tena juu ya Israel maana MUNGU alishakasirishwa na uovu wa MANASE na AMON. Yosia akawa amefanikiwa kwa kiasi kikubwa sana katika ufalme wake.

Na kwa kuwa mfalme huyu alienza kutawala akiwa na umri mdogo sana, alianza vizuri na Mungu wake, Mungu alimstarehesha sana, hakuna sehemu inayosema kuwa kuna maadui walioinuka ili wapigane na ufalme wake. Biblia inasema katika 2 Wafalme 23:25, Kabla ya huyo hapakuwa na mfalme mfano wake aliemwelekea BWANA Kwa moyo wake wote na kwa roho yake yote na kwa nguvu zake zote sawasawa na sheria zote za Musa wala baada yake hakuinuka mmoja mfano wake yeye.

Ni kweli kabisa anahitaji kupongezwa.
Sasa je mwisho wake unakuwaje?
Baada ya Mungu kumneemesha mfalme huyu, kumstarehesha kila pande, akaamua kujitia kiherehere cha kuingilia vita isiyomhusu. Ukisoma katika 2 Wafalme 23:29, Farao-neko mfalme wa Misri anainuka kupigana na mfalme wa Ashuru, haya ni mataifa mawili tofauti kabisa na israel/Yerusalemu,. Lakini Yosia akaenda ili apigane. Huyu mfalme wa Misri akamuua Yosia.
Huo ukawa mwisho wa kizembe kabisa wa mfalme Yosia ambae alianza vizuri hadi kusifiwa na Mungu.

Mpendwa mtu wa Mungu kuna mambo mengi sana kujifunza hapa:
1. Ni mambo mangapi tulianza vizuri lakini kadri siku zinavyokwenda tunatengeneza mwisho mbaya?
2. Je pale tunapogundua kuwa mwisho wetu unakuwa mbaya ni hatua gani za kuchukua?
3. Je tunabweteka na mwanzo wetu, na kujihalalishia kuwa sisi tumeshakamilika hivyo tuna uwezo wa kujiongoza wenyewe?
4. Je tuko tayari kuyaacha yale yote yanayosababisha mwisho wetu kuwa mbaya?
5. Je tunatambua kuwa Mungu anafahamu mwanzo wetu na mwisho wetu, ila ametupa "option" ya kuchagua tuanzeje na tumalizieje?
Mungu akubariki sana.
Nakutakia tafakari njema
#USIISHIE_NJIANI
Imeandikwa na
Steven Mshiu,
0655-882074
au baruapepe smshiu42@gmail.com
Oct 20, 2017

Alhamisi, 19 Oktoba 2017

PASSWORD!!!

PASSWORD/NYWILA.


Na Steven Mshiu.

Dunia ya sasa imekuwa ni ya kujihami sana, Kila kitu ambacho mtu anafanya anasisitizwa kufanya kwa umakini na kwa usiri pasipo kumwamini mtu mwingine.

Ukienda benki kufungua akaunti utahitajika kuwa na Nywila imara kwenye kufanya miamala kwa kutumia kiotomotela, Nywila hizo ni siri kubwa sana kwako na kamwe huwezi kumwambia mtu, Ni siri yako.

Huduma zote za miamala ya simu kama M-pesa, Tigo pesa n.k nayo pia ni lazima uwe na password ambazo ni siri yako. Pesa ni zako ila kama huna password imara zisizoweza kudukuliwa na watu, huwezi kuzipata pesa hizo.

Dunia nzima imekuwa ni ya Password. Kuingia kwenye mitandao ya kijamii utahitajika kuwa na password, Ukitaka kuingia Facebook, kuna sehemu utahitajika kuweka password,
Simu zetu tumeweka password kuanzia upande wa sms, majina, file manager, yani kila kitu tumekiwekea password. Dhumuni la kuweka password ni kuhakikisha usalama wa simu zetu, kuhakikisha usalama wa taarifa zetu ili zisidukuliwe au kufahamika kwa watu wengine,

Unaweza ukasahau Warumi 6:1-3 inasemaje lakini huwezi kusahau password ya kuingia facebook
Unaweza ukasahau hata kuomba asubuhi kumshukuru Mungu kwa kukuamsha tena, Lakini huwezi kusahau password ya kuingia whatsapp kuangalia ni kitu gani kimetupiwa kwenye lile group.

Maisha yetu nayo yanahitaji password. Shetani anakesha usiku na mchana kuhakikisha anayadukua maisha yetu, kama huamini soma Ayubu 1, alijaribu kuyadukua maisha ya Ayubu lakini akamkuta ana NYWILA imara.

Alipojaribu kudukua maisha ya Yesu kwenye Mathayo sura ya nne, alimkuta Yesu akiwa Na NYWILA imara,

PASSWORD ya muhimu kwa maisha ya mkristo yeyote ni NENO LA MUNGU pamoja Na MAOMBI. Password hizi ni lazima ziwe imara sana zisizoweza kudukuliwa na yeyote.
Sasa wewe kuwa bize kuweka password, kuanzia twita, insta, fb, BBM, sijui na wapi tena Halafu sahau kuwekea maisha yako PASSWORD.

Kumbuka password zaweza kudukuliwa, Ni lazima uwe na password imara,
Neno la Mungu liwe imara kwenye maisha yako.
Maombi yako ni lazima yawe imara.

Mungu akubariki sana.

Steven Mshiu.
0655 882074
0768 882074

JIKAGUE KABLA YA KUKAGULIWA

SIMAMA UKAGULIWE.
Na Steven Mshiu
Kipindi fulani nikatembelea ofisi moja hivi kwa sababu nilikuwa nina shida na boss wa ofisi hiyo.
Kwa kuwa nilikuwa na vigezo vyote vya kuonana nae sikuwa na shaka yoyote, nilijua nitanyoosha njia moja kwa moja hadi ofisini.

Lakini jambo la kusikitisha wakati naingia getini tu, nilikutana na walinzi pamoja na maneno yaliyoandikwa "SIMAMA UKAGULIWE"
Sikuwa na ubishi wowote ingawa huyo boss alinifahamu, ilinibidi nisimame nikanyoosha mikono kando huku nimesimama wima, yule mlinzi akachukua kile kimashine chake na kufanya kazi ya ukaguzi,

Kwa bahati mbaya nilikuwa nimeweka ufunguo mfukoni, kile kimashine kikaanza kupiga alarm, nikaambiwa nionyeshe kuwa nimeweka nini mfukoni, Dah, ikabidi nitoe ule ufunguo,
Akanikagua mara ya pili tena.

Ndipo nikaruhusiwa kuingia ndani, kabla sijafika ofisini kwake nilikutana na Sekretari nae akanipa kitabu cha kujaza taarifa zangu na ninataka nini kwa huyo boss, ndipo akaniruhusu niingie.
Wanadamu tunaweza kujiwekea ulinzi mkubwa sana, unaposafiri ni lazima gari ikaguliwe na SUMATRA, wale mliosafiri kwa ndege mnafahamu ukaguzi wa pale uwanja wa ndege, Huwezi kuruhusiwa kusafiri bila kufanyiwa ukaguzi.

Hivyo basi katika safari hii ya mbinguni nayo ukaguzi wake haukwepeki, Ni lazima ufanye ukaguzi wa Roho yako kila siku, Huwezi kwenda mbinguni ilhali karoho kako ni kachafu.
Haijalishi unamfahamu MUNGU kiasi gani ni lazima kila siku ufanye ukaguzi wa roho yako. Huwezi kwenda mbinguni kama utakwepa ukaguzi wa roho yako.
#USIISHIE_NJIANI
#FIKIA_USHINDI_MKUBWA

Steven Mshiu
0655 882074
0768 882074

Email: smshiu42@gmail.com
Facebook page: m.fb.com/faithtz

Jumanne, 17 Oktoba 2017

TUNZA NDOTO YAKO.




IKO WAPI NDOTO YAKO!!!?
Na Steven Mshiu
Habari mpenzi msomaji wa makala zetu. Ni uhakika wangu kuwa uko vizuri kabisa. Hata mimi pia hadi wakati huu ninapoandika makala niko njema kabisa. Hili ni jambo la kumshukuru Mungu wetu.

Leo katika mfululizo wa makala zetu nimependa kuja na swali hili, "IKO WAPI NDOTO YAKO?" Kama unavyojua sote tulizaliwa na ndoto/maono ya kufanya au kuwa na kitu fulani, lakini kadri siku zinavyokwenda zile ndoto zinapotea taratiibu.

Mfano, tukiwa wadogo kabisa wengi wetu tulitengeneza magari kwa kukata galoni, tukatumia tairi za malapa, kama sio magunzi, wengine waliona wasishindwe kabisa wakatengeneza hata baiskeli za miti. Unazikumbuka betri za ABC? Tuliziponda ponda ili tupate tairi!

Wengine tulikuwa ni mainjinia wa ujenzi, tulitumia matope kujenga nyumba tena za kifahari kama sio ghorofa. Hakuna aliekubali kushindwa. Tulikuwa na malengo ya kuwa na familia bora, yani kuoa na kuolewa. Hahah! Kibaba baba na kimama mama. Michezo yote hiyo ilikuwa ni kama unabii wa kutimiza ndoto zetu.

Tulikuwa n
a ndoto za kuwa wahubiri/­wachungaji, waalimu, n.k. lakini leo WHERE IS OUR DREAM? Hebu fanya tathmini kile ulichokuwa unakifanya ukiwa mtoto kimeenda wapi? na kwanini tumeshindwa kukitimiza? Halafu chukua hatua madhubuti.

Pengine kukosa ajira na ugumu wa maisha kumefuta ile ndoto ya kumiliki gari. Au ni watu wamekuambia kama baba yako alikufa hana hata baiskel wewe utakuwa na gari kweli? Au wamekuambia kuwa "huwezi" na wewe ukakata tamaa kabisa?

Kuzalia nyumbani kwenu kumeondoa ndoto yako ya kuwa mama bora wa familia? Ukaona huwezi tena kuolewa ukaamua kujiingiza kwenye ukahaba kabisa.? Kuishi kwenye nyumba ya kupanga na kukosa hata kakiwanja kumefuta ile ndoto yako ya kumiliki ghorofa?

Je ni TCU walibadili ndoto yako pale ulipotaka kuwa daktari wakakupangia ualimu kwa sababu wewe ni mtoto wa mkulima? Hebu fikiria kingine tena. Ok. Ulikuwa na lengo la biashara lakini kuona mwenzako kaanza biashara uliyokuwa unaiwaza ukakata tamaa, na ndoto yako ikaishia hapo?

Jifunze kwa YUSUFU katika Biblia.
Licha ya kupitia changamoto nyingi ambazo zingeweza kuizima ndoto yake hakukata tamaa. Alitambua kuwa kupitia changamoto zote hizo MUNGU aliyakusudia kuwa ni mema. Soma mwanzo 50:20. Mwishowe anakuja kuwa waziri mkuu katika nchi ile ya Misri.

Nataka ufahamu kuwa kizuizi kikubwa cha ndoto zako ni wewe mwenyewe. Jitahidi ukiondoe kikwazo hicho. Utaitimiza ndoto yako. Usihesabu pale uliposhindwa. Jitie nguvu inuka tena kwani unaweza. Dont look back look foward always.

Ninapomalizia naomba nikukumbushe mambo haya machache yatakayosababisha uzitimize ndoto zako.
1. Usimkilize mtu yeyote anaekuambia kuwa huwezi, hata kama ni mtu wako wa karibu.
2. Weka malengo kutimiza ndoto yako
3. Itangaze ndoto yako na chukua hatua kuitimiza.
4. Kila jambo unalolifanya mtangulize MUNGU kwani yeye ndio kila kitu.

Nimalizie kwa kukuambia hivi, 'YES. YOU CAN.

''OUR SUCCESS IS YOUR SUCCESS"

Mwandishi: Steven I. Mshiu
0655882074
smshiu42@gmail.com

CHUKUA HATUA LETA BADILIKO



CHUKUA HATUA KUFIKIA KILE UNACHOKIWAZA. KITALETA MAFANIKIO.

Na Steven Mshiu

Habari za wakati huu mpenzi msomaji wa makala zetu kupitia blog hii. Ni matumaini yangu kuwa u bukheri wa afya, hata mimi pia namshukuru Mungu kwa uzima alionipa..

Karibu tuendelee kujifunza na kutiana moyo kutokana na changamoto ambazo tunazipitia kila iitwapo leo katika maisha yetu. Nakutia moyo kuwa kila hali unayoipitia tambua ni kusudi la Mungu, na uamini kuwa ataifanya kuwa njema. Soma Mwanzo 50:20.

Leo katika mtiririko wa makala zetu natamani tukaangalie kuhusu KUCHUKUA HATUA KWA KILE UNACHOKIWAZA KWANI KITALETA MATOKEO MAZURI. Unajua watu waliofanikiwa katika nyanja mbalimbali hususani biashara n.k, walikuwa na wazo na walipoamua kuchukua hatua za kulitimiza wazo lao lilileta mafanikio makubwa.

Hakuna mwanadamu aliezaliwa kwa bahati mbaya. Wote tuko kwa kusudi maalum, hivyo ni lazima tuchukue hatua za kulitimiza kusudi hilo. Watu wengi wana mawazo mazuri tena yenye kuleta mafanikio lakini kutokana na ile hali ya kuog
opa na kukata tamaa, inafanya lile kusudi kutotimia. Na pia ni lazima uanze kuishi maisha ya kile unachokisudia.

 Kama una ndoto za kuwa daktari, ishi maisha ya udaktari, una ndoto za kuja kuwa mtu mkubwa katika nyanja mbalimbali, ishi maisha hayo. Itakuwa ni kituko kikubwa au ajabu la nane la dunia kama unataka kuja kuwa rais halafu tukukute kwenye vijiwe unacheza bao. Ni lazima uishi maisha ya kuja kuwa rais,. Chukua hatua.

Ukisoma katika Biblia kitabu cha 2 Wafalme 7:3-10, utakutana na habari ya wakoma wanne, ambao walikuwa wametengwa, wamenyanyapaliwa, hawathaminiwi, walipoamua kuchukua hatua na kuingia mjini, nchi ilineemeka kupitia wao.

Lakini kama wangekaa na lile wazo lao tu bila kuchukua hatua, matokeo yake wangekufa wote kwa njaa. Kumbuka kitu hiki, Mungu anasubiria wewe uanze kuchukua hatua, halafu yeye aitimilize,. hawa wakoma hawakuwa na mikono, vidole na baadhi ya viungo vingine, lakini walipochukua hatua, Mungu akafanya kule kutembea kwao kuwa mshindo mkubwa kama wa jeshi kubwa. ila walikuwa w
anne tu.

Rafiki yetu mpendwa, nikuhamasishe tu, bado hujachelewa, wakati bado upo. Hebu anza sasa kuchukua hatua kufikia kile unachokitaka. Kitaleta mafanikio. Una wazo la biashara, kufanya chochote, au hata kuandika makala kama mimi, hebu anza kuchukua hatua. Kumbuka hata mimi nilichukua hatua ya kuanza kuandika nilipopata wazo hili. Na ninaamini kuwa umejifunza mengi.

Woga wako ndio umaskini wako. Changamka chukua hatua. Dont die with your dream, make it to happen.

Ubarikiwe sana kwa kusoma makala hii. Na kama utakuwa na swali au kutaka ushauri usisite kuwasiliana nasi.

Mwandishi: Steven I. Mshiu
0655882074
Barua pepe:smshiu42@gmail.­com

WEKA TUMAINI LAKO KWA MUNGU.



UNAJUA MAHALI SAHIHI PA KUWEKA TUMAINI LAKO?

Na Steven Mshiu,
Habari mpenzi msomaji wa makala zangu. Ni matumaini yangu u bukheri wa afya, na unaendelea kujifunza mengi kupitia blog yetu hii ambayo kila siku inazidi kuwa na watembeleaji wengi. Hili linanitia moyo maana ninatambua kuwa kazi ninayoifanya sio bure.

 Tumelenga kuwafikia watu wote kwa njia mbalimbali, ikiwa ni pamoja na kuelimishana kama tunavyofanya hapa, kwa njia mbalimbali na huduma nyinginezo zinazomgusa Mungu wetu. Karibu uungane nasi.

Leo katika mfululizo wa makala zangu napenda kukushirikisha kuhusu "TUMAINI". Nianze kwa kusema hivi, Biblia inasema katika Zaburi 125:1 "Wamtumainio Bwana ni kama mlima sayuni ambao hautatikisika nao wakaa milele."

Je wewe umeweka tumaini lako wapi? Unajua tunaishi katika nyakati ambazo hatuoni tena utendaji wa Mungu katika maisha yetu, maana tumaini na tegemeo letu halipo tena kwake. Tumekuwa ni watu wa kutegemea akili zetu wenyewe. Hatujali tena chanzo cha maarifa yetu. Mahali fulani Biblia ikasema, Na kama walivyokataa kuwa na Mungu katika fahamu zao, nae aliwaacha wafuate akili zao zisizofaa. Kumbe akili zetu pasipo ni bure kabisa. Warumi 1:28

Hivi karibuni tumekuwa tukishuhudia mauaji ya kinyama kabisa kwa albino na mambo ya ajabu ajabu tu. Kwanini? Wale wanofanya hivyo si kwamba hawajui, lakini kwa sababu kuna mganga amemwambia afanye hivyo basi tumaini lake ameliweka kwa huyo mganga. Fikiria ni kiongozi wa nchi halafu tumaini lake ni kwa waganga na wachawi, halafu anataka aongoze nchi. Inawezekana? Mungu hawezi kukupa nafasi hiyo hata siku moja maana ameshakuacha ufuate akili yako isiyofaa.

Ndugu mpendwa, mahali sahihi pa kuweka tumaini lako ni kwa mungu tu. Soma mithali 16:3 mkabidhi mungu njia zako na mawazo yako yatathibitika. Haijalishi umemaliza chuo miaka minne imepita bado hujapata ajira, mtumaini mungu,. Umeanzisha biashara, haiendi vizuri. Usiende kwa mganga. Kila unalolifanya haliendi, mtumaini MUNGU tu.

Nikutie moyo, bado hujachelewa. Una nafasi ya kufanya mambo makubwa tena makubwa sana. Tambua
kuwa mafanikio yako yanategemea ni wapi ulipoweka tumaini lako. Ilipo hazina ya mtu ndipo na moyo wake ulipo. Mafanikio yanayopatikana kirahisi(kwa waganga) hayadumu. Yale yanayotoka kwa MUNGU huwa ni ya baraka sana.. Jifunze kwa "super nation" Marekani,. Kwenye dolla yao utaona rais amenyoosha mkono juu halafu kuna maandishi haya, "IN GOD WE TRUST"

Ndio maana taifa hilo kubwa duniani linaendelea kubaki katika ubora wake, mataifa mengi yanalitegemea kwa njia moja au nyingine. Thamani ya pesa yao iko juu. Kwanini? Wametambua kuwa tumaini na tegemeo lao linastahili kuwa kwa MUNGU.

Nimalizie hivi kwa leo. Unapomtegemea au kuweka tumaini lako kwa mtu au kitu mfano wachawi, waganga, ushirikina n.k, hauna tofauti na kutegemea jino lililovunjika, siku ukiletewa nyama yenye mifupa utabaki unaikodolea macho tu.

Weka tumaini lako kwa MUNGU wako rafiki.
Ahsante na ubarikiwe sana.
Kumbuka: "OUR SUCCESS IS YOURS"

Mwandishi: Steven I. Mshiu
0655882074
smshiu42@gmail.com.

UJIONAVYO NDIVYO UTAKAVYOKUWA



UJIONAVYO NDIVYO UTAKAVYOKUWA..

Na Steven Mshiu,
Habari mpenzi msomaji wa makala zangu. Ni matumaini yangu kuwa u bukheri wa afya na muendelezo mzuri katika kujenga taifa ambalo bado kwa njia moja au nyingine linaonekana kutoimarika. Nikutie moyo kuwa kazi yako ni njema na ina thawabu kwani huwezi kulima shamba leo na uvune leo leo.

Leo katika mfululizo wa makala zangu ninakuletea makala hii, "UJIONAVYO NDIVYO UTAKAVYOKUWA" Kama unavyojua kuwa kabla mtu hajafanya jambo/kitu fulani huwa kuna hali inayoanza kujijenga ndani yake, yaweza kuwa kushindwa au kushinda, kujidharau, au kijiona jasiri n.k.

Kumbuka hakuna mwanadamu alieumbiwa kushindwa, kujidharau, au kukata tamaa, sema ni zile changamoto tunazokutana nazo zinatupelekea kuingia katika hali hiyo. Hivyo ni lazima ukabiliane nayo na usikubali ikushinde.

Tukisoma katika Biblia tunaona kuwa ilifika mahali katika safari ya wana wa Israel kwenda Kanaani, wamekaribia kabisa MUNGU anamwambia Musa atume watu 12 wakaipeleleze nchi ya Kanaani, miongoni mwao yupo JOSHUA na KALEBU.

Na walipofika kuipeleleza nchi ya kanaani walikuta ina kila kitu, maziwa, asali, zabibu nk, hivyo walikuwa na kila sababu ya kuimiliki nchi ile.

Lakini tatizo walilokutana nalo ni uimara wa mji ule pamoja na watu wanaokaa katika nchi ile ndio waliowakatisha tamaa na kujidharau kuwa hawawezi kuirithi nchi ile ambayo MUNGU alikuwa amewaahidi.
 

Ona wanavyosema katika Kutoka 13:33 kisha huko tuliwaona Wanefili wana wa Anaki....."tukajiona­ nafsi zetu kama mapanzi" "nao ndivyo walivyotuona sisi"

Lakini Kalebu na Yoshua wanawatia moyo watu kuwa wapande na kuimiliki nchi hiyo, na kwa sababu wameshaathirika kisaikolojia wakajiona kuwa hawawezi kabisa. Matokeo yake wote wanafia pale jangwani, lakini Yoshua na Kalebu wao wanairithi nchi.

Je wewe unajionaje, unaona kushindwa au kukata tamaa? Inuka endelea na mapambano.


Ubarikiwe sana.
Imeandaliwa na
Steven I. Mshiu
0655882074
smshiu42@gmail.com,

MAKUNDI MAWILI YA WATU WANAOKUZUNGUKA.

FAHAMU MAKUNDI MAWILI YA WATU KATIKA MAISHA YAKO. Na Steven Mshiu . Maisha ya kila mwanadamu yamezungukwa na watu. Watu hawa waweza kat...